Rais Paul Kagame wa Rwanda, ambaye amekuweko madarakani tangu yalipohitimishwa mauaji ya kimbari nchini humo mwaka 1994, amedokeza kuwa a...
Rais Paul Kagame wa Rwanda, ambaye amekuweko madarakani tangu yalipohitimishwa mauaji ya kimbari nchini humo mwaka 1994, amedokeza kuwa atagombea tena urais katika uchaguzi unaotazamiwa kufanyika 2024.
Alipoulizwa katika mahojiano na televisheni ya France 24 kama atawania tena kiti cha urais katika uchaguzi ujao, Kagame amesema: "Ninafikiria kugombea kwa miaka 20 mingine. Sina tatizo juu ya hilo". Rais huyo wa Rwanda ameongezea kusema, uchaguzi unahusu chaguo wanalofanya watu.
Kagame aliifanyia mabadiliko katiba ya Rwanda mwaka 2015 na hivyo kumfungulia njia ya kuweza kubaki madarakani hadi 2034.
Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 64 alishinda uchaguzi wa rais wa 2017 kwa asilimia 99 ya kura kulingana na matokeo rasmi.
Paul Kagame, alikuwa na umri wa miaka 36 tu wakati harakati yake ya Rwanda Patriotic Front (RPF) ilipowatimua Wahutu wenye misimamo ambao wanalaumiwa kuhusika na mauaji ya kimbari yaliyotokea kuanzia Aprili hadi Julai 1994 na kusababisha watu wasiopungua laki nane kuuawa, wengi wao wakiwa ni Watutsi.
Licha ya kuandamwa na tuhuma za ukiukaji wa haki za binadamu, Rais wa Rwanda ametetea vikali rekodi ya serikali yake katika suala hilo pamoja na uhuru wa kisiasa alipohutubia mkutano wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola, Commonwealth uliofanyika katika mji mkuu wa nchi hiyo Kikgali mwishoni mwa mwezi uliopita wa Juni.../
Credit: MPEKUZI
Thanks for your time please share with your friends
COMMENTS