MAMBO YALIYOPELEKEA KUIBUKA KWA RIWAYA YA KISWAHILI Kabla ya kuchambua juu ya mambo yaliyosababisha kuibuka kwa riwaya ya Kis...
MAMBO YALIYOPELEKEA KUIBUKA KWA RIWAYA YA
KISWAHILI
Kabla ya kuchambua juu ya mambo yaliyosababisha kuibuka kwa riwaya
ya Kiswahili ni muhimu kuanza kuangalia maana ya riwaya. Kuna wataalamu
mbalimbali ambao wamefasili riwaya kwa mitazamo mbalimbali kama ifuatavyo;
Kwa mujibu wa Senkoro (2011) katika
kitabu chake cha Fasihi Andishi anafasili riwaya ni kisa ambacho urefu wake
unakiruhusu kitambe na kutambaa mahali pengi na kuambaa vizingiti vingi vya
maisha kama apendavyo mwandishi wake. Anaendelea kueleza kuwa riwaya ni hadithi ndefu ya kubuni yenye visa vingi,
wahusika zaidi ya mmoja na yenye mazungumzo na maelezo yanayozingatia kwa
undani na upana maisha ya jamii. Pia Wamitila
(2003), ameeleza kuwa riwaya ni kazi ya kinathali au bunilizi ambayo huwa na urefu
wa kutosha, msuko uliojengeka vizuri, wahusika wengi walioelezwa kwa kina na
yenye kuchukua muda mwigi katika maandalizi na huhusisha mandhari maalumu.
Vilevile Muhando na Balisidya (1976:76) wanasema, riwaya ni kazi ya kubuni,
hadithi ambayo hutungwa kufuatana na uwezo wa fanani kuibusha mambo kutokana na
mazoea au mazingira yake. Anaendelea kueleza kuwa riwaya yaweza kuanzia maneno
elfu 35 na kuendelea.
Kwa ujumla riwaya ni hadithi ya
kubuni yenye visa na matukio yenye mawanda mapana kwa kufungamana na wakati pia
kusawiri maisha ya jamii husika. Vilevile riwaya ya Kiswahili ni ile ambayo inafungamana na utamaduni wa Waswahili katika lugha ya Kiswahili, pia ni riwaya inayohusu Waswahili wenyewe. Baada ya kuangalia maana mbalimbali za riwaya tupige hatua na kuchambua mambo mbalimbali yaliyosababisha kuibuka kwa riwaya ya Kiswahili. Kuna wataalamu mbalimbali ambao wamejaribu kuelezea kuibuka au kutokea kwa riwaya ya Kiswahili baadhi yao ni;
Madumulla (2009) anayeeleza kuwa
riwaya ya Kiswahili ilitokana na nathari bunifu simulizi kama vile hadithi,
hekaya, ngano zilizosimuliwa kwa mdomo, pia anaendelea kusema kuwa riwaya
ilitokana na maandiko ya fani ya ushairi hususani tendi za Kiswahili.Naye Senkoro (2011), ameeleza kuwa riwaya zilizuka kutokana na
maendeleo na mageuzi ya kiutamaduni, uchangamano wa maisha ya kijamii, kisiasa,
kiuchumi na kiutamaduni yaliyopelekea haja ya kimaudhui zaidi ya ngano na
hadithi fupi.
Pia Mulokozi (1996) ameleza kuwa
chimbuko la riwaya ya Kiswahili lipo katika mambo makuu mawili ambayo ni fani
za kijadi za fasihi pamoja na mazingira
ya kijamii.
Kutokana na wataalamu mbalimbali
kuelezea kuhusiana na kuibuka kwa riwaya ya Kiswahili ambapo wote wanafungamana
katika mambo makuu mawili ambayo ni riwaya ya Kiswahili imeibuka kutokana na
fani za kijadi ambazo ni ngano, visakale, hekaya, sira, masimulizi ya wasafiri,
visasuli, visasili nk. Pamoja na maendeleo mbalimbali ya jamii, mfano maendeleo
ya kiuchumi au mazingira ya jamii. Kwa kuanza na uchambuzi wa fani za kijadi,
fani za kijadi ni mapokeo au masimulizi
ambayo yalikuwepo hata kabla ya kuja kwa fani ya maandishi. Fani hizo zilipelekea kuibuka kwa riwaya ya
Kiswahili kama ifuatavyo;
Ngano ni hadithi za kubuni ambazo
zinahusu wanyama, wanadamu, mazimwi, majini na malaika. Ngano nyingi zina msuko
sahili ambao huwasilisha kwa urahisi ujumbe uliokusudiwa. Hivyo kuna ushahidi
wa kutosha kusema kuwa riwaya
ya Kiswahili imetokana na ngano kwa sababu riwaya hufanana na ngano
kifani hasa katika wahusika na hata
katika msuko wa visa na pia katika maudhui hasa dhamira huwa zinalingana na
zile za ngano. Mfano wa riwaya hizo ni kama vile za Shaban Robert Adili na
Nduguze (Macmillan 1952) na Kusadikika. Mafano katika riwaya ya Kusadikika kuna
mhusika Ndege kwa jina lingine Mangera ambaye ni ndege mkubwa kabisa walishao katika
ardhi lakini walalao kusadikika, hivyo
ndege huyu alitumiwa na Mjumbe wa kusadikika
Amini aliyetumwa ardhini alijifunga juu ya paja la Mangera usiku na asubuhi
ndege alienda ardhini na Amini nae akiwa
kwenye paja la Mangera alijifungua baada ya kufika ardhini akatembea baada ya kumaliza mambo
yake akenda tena kwa yule ndege
akajifunga tena na usiku ulipofika
wakaenda kusadikika. Hivyo athari za ngano katika riwaya ya Kiswahili ya leo tunaziona katika muundo sahili wahusika wengi ni bapa
na lengo ni kutoa maadili.
Hekaya ni hadithi za kusisimua
kuhusu masahibu na matukio ya ajabu na
yasiyokuwa ya kawaida. Mfano mzuri wa hekaya ni zile za Alfu-lela-Ulela hekaya
za Abunuasi, hekaya hizi zilienea kabla hata ya ujio wa wakoloni. Hivyo kuna
mfanano mkubwa sana wa kifani na wa
kimaudhui na riwaya za Kiswahili. Mfano wa riwaya za Kiswahili zilizotokana na
hekaya ni Adili na Nduguze ya Shaban Robert ( Macmillan 1992) na Ubeberu
Utashindwa ya Kimbila (TUKI 1997). Hizi
zote zimeathiriwa na hekaya za kijadi, hivyo ndio maana tunasema riwaya za
Kiswahili zimetokana na fani za jadi.
Sira ni masimulizi ya kweli kuhusu
maisha ya mtu. Sira zinaweza kuwa wasifu, habari za mtu kusimuliwa na mtu
mwingine au tawasifu mtu anajisimulia yeye
mwenyewe kuhusu maisha yake. Sira iliathiri kuibuka kwa riwaya kwani masimulizi
ya kisira yalikuwapo katika fasihi simulizi, pia katika maandishi ya Kiswahili
tangu zamani, kabla ya ukoloni yalikuwapo
maandishi yaliyohusu maisha ya Mitume na Masahaba. Mfano Hemed Bin
Muhammed(1902) aliandika maisha ya Hemed Bin Muhhamed el Murjebi yaani Tippu
Tip kwa maneno yake mwenyewe. Hivyo tunaona kuna mfanano wa kimaudhui na riwya
za Kiswahili. Mfano wa riwaya hizo ni zile za Shaban Robert Maisha Yangu (Nelson 1949) na Wasifu wa Siti
binti Saad ( TALL 1958) na pia Rosa Mistika ya
E. Kezilahabi, (EALB 1971).
Tendi ni ushairi simulizi ambao kwa kawaida ni
mrefu na hueleza sifa mbalimbali za mashujaa. Mfano Utendi wa Fumo Liyongo ya Mohamed
Kijumwa (1913), utendi wa Sundiata na au tendi wa vita vya Wadachi Kutamalaki
Milima- Hemedi Abdulah (1985). Jadi hizi zilipelekea kuibuka kwa riwaya za
kitendi, mfano Kadagaa Kamemwozea, Moto wa Mianzi ambayo ilizungumzia Wahehe na
mtemi wao Mkwawa. Pia kuna mfanano
mkumbwa katika fani na maudhui ya tendi za kijadi na riwaya za Kiswahili ambapo
maudhui ya tendi za kijadi yalikuwa yamelenga kuelezea sifa za mashujaa mbalimbali
vilevile na riwaya za Kiswahil baadhi zipo zinazoelezea sifa mbalimbali za
mashujaa.
Visasili ni hadithi zinazoelezea
chimbuko au asili ya watu, vitu, mataifa, na pia uhusiano wa wanadamu pamoja na
mizimu. Zipo riwaya ambazo ziliibuka
kutokana na visasili mfano riwaya ya Lila na Fila (Kimbila 1966) ambayo ilikopi
motifu ya ziwa Ikimba huko Bukoba, pia hadithi ya Mungu wa Wakikuyu na Malimba Majaliwa (E.Semzaba) nazo zinaelezea asili ya
vitu mbalimbali.
Visakale ni hadithi za kale kuhusu
mashujaa wa taifa au dini. Mara nyingi visakale huchanganya historia na
masimulizi ya kubuni. Mfano kulikuwa na hadithi ya chimbuko la mji wa pwani,
Mijikenda na Mwinyi Mkuu wa Zanzibar.
Visa hivi vilipelekea kuibuka kwa riwaya kama Habari za Wakilindi (Abdalah Bin
Hemed Ally Ajjemy 1972), Kisima cha Giningi ya M.S. Abdula (1968) na pia Hadithi ya
Myombokele na Bibi Bugonoka.
Baada ya kuangalia jinsi fani za
kijadi zilivyopelekea kuibuka kwa riwaya ya Kiswahili zifuatazo ni hoja zinazoonesha jinsi maendeleo mbalimbali ya jamii au mazingira ya
jamii yalivyopelekea kuibuka kwa riwaya ya Kiswahili.
Kugunduliwa kwa hati za maandishi, kabla ya
ujio wa wakoloni Afrika mashariki hususani Tanzania haikupata kuwa na hati za
maandishi, lakini baada ya kuja kwa Waarabu
walileta hati za kiarabu lakini hata hivyo hazikutumika katika riwaya kwa
sababu hawakuwa na utamaduni wa riwaya kwa hiyo hawakuleta athari yoyote katika
riwaya bali athari za hati ya maandishi ya waarabu zilijitokeza katika ushairi
wa Kiswahili. Hivyo basi baada ya kuja kwa wakoloni wa kizungu walileta hati za
kirumi ambazo zilileta athari kubwa katika riwaya ya Kiswahili. Kwani watu walijifunza kuandika hati hizo za kirumi na
kuzitumia katika kuandika riwaya ya Kiswahili. Mfano riwaya ya Safari za Waswahili,
Habari za Wakilindi, Uhuru wa Watumwa ya J. Mbotela (1934). Riwaya hizi za
kiswahili ziliandikwa baada ya kugunduliwa kwa hati za maandishi.
Pia kuwapo kwa teknolojia ya
urudufishaji na usambazaji, ugunduzi huu wa teknolojia ya upigaji chapa vitabu uligunduliwa na
Johannes Gutenberg huko Ujerumani mwaka 1450. Ugunduzi huu ulirahisisha kazi ya
uchapaji vitabu katika nakala nyingi na kuondoa kabisa hali ya kunakili kwa
mikono. Teknolojia hii ilienea Afrika mashariki baada ya ujio wa wakoloni
ambapo ilisaidia kuibuka kwa uchapaji na usambazaji wa riwaya za Kiswahili.
Mfano 1948 kulianzishwa shirika la vitabu Afrika mashariki (EALB) ambapo
lilirahisisha uchapaji wa kazi mbalimbali za riwaya za Kiswahili. Mfano Mzimu
wa Watu wa Kale (1960) na Kurwa na Doto
(1960).
Vilevile ukuaji mkubwa wa kiuchumi, uchumi mkubwa
ulisaidia kuibuka kwa riwaya ya Kiswahili kutokana na kuwapo kwa tabaka la watu
wenye pesa ambao waliweza kununua vitabu vingi vya riwaya na kujisomea. Hii
ilipelekea uzalishaji mwingi wa vitabu vya riwaya ya Kiswahili kwa ajili ya kuwaburudisha pia kutokana na
uhakika wa soko riwaya nyingi zilizalishwa kwa wingi zaidi. Mfano katika
kipindi cha ukoloni ambapo wakoloni walikuwa na uchumi uliotengemaa hivyo
hawakuwa na kazi za kufanya kwa sababu kazi zao nyingi zilifanywa na waafrika.
Hivyo walipata muda mwingi wa kusoma vitabu vya riwaya kutokana na hali hiyo
ilipelekea kuibuka kwa riwaya nyingi zaidi.
Kuwapo kwa mfumo rasmi wa elimu,
mfumo huu uliletwa na wakoloni wa Kiingereza na Kijerumani ambao walianzisha shule
mbalimbali zilizosaidia watu wengi
kujifunza kusoma na kuandika. Kwa hivyo watu waliojifunza kusoma na
kuandika, waliandika na kusoma riwaya
kwa wingi kitu ambacho kilipeleke kuibuka kwa riwaya nyingi za Kiswahili. Mfano
Kusadikika, Uhuru wa Watumwa, Kufikirika, Adili na Nduguze. Hivyo
basi inaonesha kuwa kadiri elimu ilivyopanuka na ndivyo wasomaji na waandishi wa
vitabu vya riwaya walivyoongezeka na kufanya kuwepo hadhira kubwa nzuri ya
wasomaji na watunzi wa riwaya ya Kiswahili.
Vilevile kuwapo kwa maskani ya kudumu, kwa
mtu anayeishi maisha ya kuhamahama ni
vigumu sana kujijengea jadi ya kusoma, hawapati fursa ya kukaa na kuweza kusoma
na kuandika. Muda mrefu wa mchana
hutumika katika kuchunga mifugo yao, kurina asali, kuwinda, kusaka na
kukusanya matunda na mizizi kwa ajili ya chakula hivyo hawapati fursa nzuri ya kujishughulisha
na elimu ya kusoma na kuandika hivyo kwao riwaya ni kitu kigeni. Baada ya
kuwepo kwa maskani ya kudumu watu walipata fursa nzuri ya kusoma na kuandika.
Hii ikawasaidia kuandika na kusoma riwaya kwa wingi na kupelekea kuibuka kwa
riwaya ya Kiswahili.
Kwa kuhitimisha tunaweza kusema kwamba, japokuwa kuibuka kwa riwaya ya
Kiswahili kumetokana na mambo makuu mawili ambayo ni fani za kijadi na mazingira
ya jamii lakini inayoonesha mashiko zaidi ni ile ya maendeleo mbalimbali ya
jamii au mazingira ya jamii,kwa sababu jamii inavyozidi kuendelea katika nyanja
mbalimbali inapelekea riwaya kuandikwa
kwa wingi kutokana na kuongezeka kwa waandishi au watunzi na wasomaji wa riwaya
hizo.
Madumulla,J.S
(2009). Riwaya ya Kiswahili,Historia ya Misingi
ya Uchambuzi, Nairobi: Sitima
printer and station Ltd.
Mhando,
P na Balisidya (1976). Fasihi na sanaa za
maonyesho, Dar es salaam: Tanzania
publishing house.
Mulokozi,
M.M (1996). Utangulizi wa Fasihi ya
Kiswahili, Dar es salaam: TUKI.
Senkoro,
F.E.M.K (2011). Fasihi Andishi, Dar
es salaam: Kauttu Ltd
COMMENTS